Jumamosi, 14 Julai 2018

FASIHI LINGANISHI---Mchango wa Tafsiri katika Fasihi ya Kiswahili


CHUO KIKUU KISHIRIKI CHA ASKOFU MKUU YAKOBO
                                                                                              
KITIVO CHA SANAA NA SAYANSI ZA JAMII
IDARA YA LUGHA, ISIMU NA FASIHI
 JINA LA KOZI:                     FASIHI LINGANISHI YA KISWAHILI
 MSIMBO WA KOZI:           SW 338
 JINA LA MHADHIRI:         MIGODELA, W.
 AINA YA KAZI:                   KAZI YA KIKUNDI
 KUNDI NAMBA:                 2
 WASHIRIKI
S/N.
               JINA
NAMBA YA USAJILI
SAHIHI
01.
CYPRIAN SIMEO, S
45289

02.
KANANI EUGENIA
45325

03
KWILASA DANIEL
45343

04.
MWAIPONJ A ANNE
45387

05.
MWAKYANDO SAMWEL
45391

06.
PONERA JESKA, L
45428

07.
TAMIMU RAJABU, A.
45447

08.
MUNG’ONG’O WITNESS
45466

09.
MBIJIMA VICTOR
45506

SWALI;
Mchango wa Tafsiri katika Fasihi ya Kiswahili.


Utangulizi
Dhana ya Tafsiri na Fasihi Linganishi kwa mujibu wa wataalamu mbalimbali.
Mwansoko na wenzake (2006) wanafasili Tafsiri kuwa ni zoezi la uhawilishaji wa mawazo katika maandishi kutoka lugha moja hadi nyingine.
As-safi akimnukuu Dubois (1974) anaeleza kuwa Tafsiri ni uelezaji katika lugha nyingine au lugha lengwa wa kile kilichoelezwa katika lugha nyingine (lugha chanzi) ikihifadhi maana na mtindo wa matini chanzi.
Catford (1965:20) anasema tafsiri ni kuchukua mawazo yaliyo katika maandishi kutoka lugha moja (lugha chanzi) na kuweka badala yake mawazo yanayolingana katika lugha nyingine (lugha lengwa).
Boldor (2003) akimrejelea Compbell (1926) Fasihi Linganishi ni taaluma inayochunguza uhusianao uliopo baina ya fasihi mbili au zaidi nje ya mipaka ya kitaifa kwa njia ya kulinganisha mfanano na msigano
Henry Remak (1971) anafasili Fasihi Linganishi kama uwanja wa kifasihi unaohusika na uchunguzi na mahusianao ya kifasihi nje ya mipaka ya nchi moja, pia kati ya fasihi na fani nyinginezo. Kwa maelezo haya ya Remak tunachoweza kusema ni kwamba Fasihi Linganishi haiishii kuangalia mahusino ya kifasihi peke yake bali huangalia mahusiano kati ya fasihi na fani nyinginezo zisizo za kifasihi.
Wamitila (2003) anaeleza kuwa fasihi linganishi  inahusu uchambuzi wa maandishi ya wakati mmoja na aina moja na katika lugha mbalimbali kwa  nia ya kumiliki sifa zinazoyahusisha  kama athari, vyanzo, sifa zinazofanana na tofauti za kiutamaduni. Anaendelea kueleza kuwa inawezekana kufanya hivi kwa nia ya kuangalia matapo mbalimbali, maendeleo au hata nadharia za kiuhakiki. Fasihi ya namna hii iliweka misingi na juhudi za wanaisimu kuanza kuilinganisha lugha mbalimbali katika karne ya kumi na tisa.
Kutokana na fasili zote hizo kuhusu tafsiri tunaweza kuhitimisha kwa kusema kuwa, tafsiri ni uhawilishaji wa mawazo, ujumbe au taarifa iliyopo katika maandishi kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa bila kupoteza maana ya msingi na mtindo uliotumika katika matini chanzi. Na maana katika tafsiri inatakiwa iendane na lengo la mtunzi wa matini chanzi lakini pia kwa kuzingatia utamaduni wa jamii unayoitafsiriya.
Pia Fasihi Linganishi ni aina ya fasihi ambayo inajikita zaidi kutumia mbinu za kiulinganishi baina ya kazi mbili za kifasihi ili kujua sifa fulani fulani kama vile kufanana kwa kazi hizo, tofauti za kiutamaduni katika kazi hizo, kujua ulinganishi katika lugha yaani sarufi ya lugha katika kazi hizo za kifasihi.
Historia na Maendeleo ya Tafsiri nchini Tanzania.
Wanjala (2011) anaeleza kuwa, historia ya tafsiri imeangaliwa kwa kuegemea vipindi muhimu vya maendeleo na mabadiliko ya elimu na utamaduni. Nchini Tanzania, tafsiri haina historia ndefu sana kwani imeanzia mnamo karne ya 19 na inaweza kugaiwa katika vipindi vitatu vikuu navyo ni kabla ya utawala wa kikoloni, wakati wa utawala wa kikoloni na baada ya uhuru.
Kabla ya utawala wa kikoloni
Kabla ya utawala wa kikoloni wamishionari walitafsiri vitabu mbalimbali vya kikristo ikiwemo Biblia Takatifu kutoka lugha ya Kiingereza kwenda Kiswahili na lugha nyingine za makabila kwa lengo la kueneza dini na ustaarabu wa kikristo kwa waafrika.

Kipindi cha Ukoloni
Hiki ni kipindi kuanzia miaka ya 1800, katika kipindi hiki, wakoloni hasa waingereza walitafsiri maandiko mbalimbali ya kitaaluma na fasihi ya Ulaya kwa lugha ya Kiswahili. Vile vile kabla ya uhuru zipo baadhi ya kazi za fasihi zilizotafsiriwa na watanzania. Kwa mfano tamthiliya ya MZIMU WA WATU WA KALE iliyotafsiriwa na Mohammed Said Abdalla (1960) kutoka lugha ya kiingereza Shrine of The Ancestors.
Baada ya Uhuru
Baada ya uhuru ambapo ni kuanzia mwaka 1961. Katika kipindi hiki wapo wataalamu waliofanya juhudi za kutafsiri vitabu mbalimbali kwa lugha ya Kiswahili. Mfano mzuri ni Mwalimu Julius K. Nyerere ambaye alitafsiri vitabu viwili vya mwandishi mashuhuri wa Tamthiliya wa huko Uingereza aitwaye William Shakespeare ambavyo ni tamthiliya ya JULIUS KAIZARI (Julius Caesar, 1963) na tamthiliya ya MABEPARI WA VENIS (The Merchant of Venis, 1969). Kazi nyingine zilizotafsiriwa baada ya uhuru ni WIMBO WA LAWINO (Song of Lawino) iliyotafsiriwa na Paul Sozigwa (1975), riwaya ya UHURU WA WATUMWA (The Freeing of the Slaves in East Africa) iliyotafsiriwa na East African Literature Bureau (1967), NITAOLEWA NIKIPENDA (I Will Marry When I Want) iliyotafsiriwa na Crement M. Kabugi (1982).
Kwa ujumla maendeleo ya taaluma ya tafsiri nchini Tanzania yamepiga hatua kubwa kutokana na kukua kwa sayansi na teknolojia. Taaluma ya tafsiri inafundishwa katika elimu ya sekondari na katika vyuo vikuu mbalimbali. Pia taasisi na asasi zinazojishughulisha na tafsiri zimeongezeka kwa mfano Baraza la Kiswahili la Zanzibar (BAKIZA), Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni (TAKILUKI) na Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA).

Mchango wa Tafsri katika Fasihi ya Kiswahili.
Tafsiri imesaidia katika kueneza dini na vipengele vingine vya utamaduni kutoka mataifa ya nje. Tafsiri ni nyenzo ya kuenezea utamaduni kutoka taifa moja kwenda jengine au kutoka jamii moja kwenda nyingine. Kwa mfano kutokana na Wazungu kutafsiri Biblia na Waarabu kutafsiri Kur-An kwa lugha ya Kiswahili, kulisababisha waafrika kwa ujumla kubadilisha dini zao za kijadi na kufuata dini ya Ukristo na Uislamu.
Tafsiri imesaidia katika kukuza lugha na fasihi ya Kiswahili. Lugha ya Kiswahili ni miongoni mwa vipengele muhimu sana katika utamaduni wa Tanzania kwa sababu Kiswahili ni lugha rasmi, lugha ya taifa na Tunu ya taifa. Kabla ya kuwepo taaluma ya Tafsiri, lugha ya Kiswahili ilionekana kudumaa hasa katika nyanja ya sayansi na teknolojia. Lakini baada ya kuwepo taaluma hii, wataalamu na Taasisi mbalimbali za Kiswahili zimekuwa zikifanya jitihada za kutafsiri vitabu vya lugha mbalimbali kwenda lugha ya Kiswahili pamoja na kutafuta Istilahi na Misamiati ya Kiswahili inayoweza kwenda sambamba na Istilahi za Kisayansi. Mfano wa istilahi hizo ni kama vile Password – Nywila, Keyboard – Kicharazio, Scanner – Mdaki, Flash Disc – Diski Mweko na Mouse – Kiteuzi.
Tafsiri ilisaidia kuongeza hamasa ya usomaji wa kazi za kifasihi. Historia inaeleza kuwa, wakati wa ukoloni fasihi ilidumaa kwa sababu Waafrika hawakuwa na mwamko wa kusoma vitabu na kazi nyingi za kifasihi ziliandikwa kwa lugha ya Kiingereza kwa lengo la kuwafurahisha Mabwana. Lakini baada ya wataalamu wa fasihi kuanza kutafsiri kazi mbalimbali za fasihi ya Ulaya kwa lugha ya Kiswahili na lugha nyingine za makabila mwamko wa kusoma vitabu uliongezeka. Mfano wa vitabu vya fasihi vilivyotafsiriwa wakati wa ukoloni ni MZIMU WA WATU WA KALE (Shrine of the Ancestors) iliyotafsiriwa na Mohammed Said Abdalla (1960). Pia kuna kazi mbalimbali za kifasihi zilizotafsiriwa baada ya uhuru, miongoni mwao ni Juliasi Kaizari (Julius Caesar) (1963) na MABEPARI WA VENIS (The Merchant of Venis) (1967), zote hizo zimetafsiriwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Baada ya hapo kazi mbalimbali za kifasihi kama vile hadithi fupi, Riwaya, Tamthilia na Mashairi yalitafsiriwa kutoka lugha mbalimbali kwenda katika lugha Kiswahili. Vile vile kazi za fasihi ya Tanzania zilitungwa na kupelekea kukua na kuenea fasihi ya Kiswahili.
Tafsiri imesaidia katika kukuza elimu nchini Tanzania. Elimu ikiwa ni sehemu ya utamaduni wa Tanzania, imepiga hatua kutokana na maendeleo ya mitaala na mbinu mbalimbali za kufundishia. Tafsiri ni miongoni mwa mbinu inayotumiwa na walimu wengi ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wanafikia lengo la kujifunza kwa mujibu wa viwango vyao. Juhudi mbalimbali zinachukuliwa katika kukuza elimu ya Tanzania. Miongoni mwa juhudi hizo ni kutafsiriwa kwa vitabu vya masomo mbalimbali ili visaidie katika marejeleo. Vile vile taaluma ya tafsiri imekuwa ni kozi muhimu katika shule za sekondari na vyuoni ili kuwapa wanafunzi uwezo wa kuitumia taaluma hii ili waweze kujiajiri kwa kutafsiri kazi mbalimbali.
Tafsiri imesaidia katika kuibua nadharia mpya ya Fasihi Linganishi. Kama ijulikanavyo kuwa fasihi ni sanaa na sanaa ni sehemu ya utamaduni. Kwa mujibu wa kitabu cha “Utangulizi wa Nadharia ya Fasihi Linganishi” kilichoandikwa na Athumani S. Ponera (2014) ni kwamba, lengo la nadharia hii ni kuchunguza kufanana na kutofautiana kati ya fasihi ya Tanzania na fasihi ya mataifa mengine hasa Amerika na Ulaya na hata kazi za mwandishi mmoja na mwandishi mwingine au kazi tofauti za mwandishi mmoja hususani katika vipengele mbalimbali vya utamaduni pamoja na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Kwa hiyo kutokana na maelezo hayo ni wazi kuwa kuwepo kwa kazi nyingi za mataifa ya nje zilizofasiriwa kwa lugha ya Kiswahili na zile ambazo hazijafasiriwa ni sababu tosha iliyomsukuma mwandishi kuanzisha mjadala huu wa nadharia mpya ya fasihi linganishi kama ilivyo kwa nadharia ya isimu linganishi.
Tafsiri imesaidia katika kukuza biashara na kuinua uchumi wa Taifa. Kama tulivyotangulia kusema kuwa, utamaduni ni utu na utu ni muhimu katika maisha ya watu. Biashara ni miongoni mwa sekta inayounganisha watu wa aina tofauti.  Kuwepo kwa utu katika biashara ndio kutasaidia kukuza biashara na uchumi wa nchi yetu. Mchango wa tafsiri katika biashara ni kuwa mikataba mingi ya biashara na uwekezaji nchini Tanzania inatafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili ili kuwawezesha wananchi kupata haki zao. Vile vile matangazo mbalimbali ya kibiashara na taarifa nyingine katika vyombo vya habari kama vile magazeti hutafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili ili kila mwananchi apate kufaidika na huduma zinazotolewa.
Tafsiri imesaidia kuingiza utanzu mpya wa Fasihi Andishi katika fasihi ya Kiswahili. Hapo mwanzo kabla ya tafsri, Fasihi ya Kiswahili haikuwa na utanzu wa Tamthiliya lakini kwa kutumia tafsiri hivi sasa Tamthiliya ni moja kati ya tanzu muhimu katika Fasihi ya Kiswahili. Mifano ya Tamthiliya zilizo tafsiriwa ni pamoja na tamthiliya ya JULIUS KAIZARI (Julius Caesar, 1963) na tamthiliya ya MABEPARI WA VENIS (The Merchant of Venis, 1969), WIMBO WA LAWINO (Song of Lawino) iliyotafsiriwa na Paul Sozigwa (1975), NITAOLEWA NIKIPENDA (I Will Marry When I Want) iliyotafsiriwa na Crement M. Kabugi (1982).
Vilevile tafsiri imesaidia kueneza Fasihi ya Kiswahili na utamaduni wake, kuna kazi za fasihi ya Kiswahili zilizotafsiriwa kwa lugha nyingine za kigeni kwa mfano Riwaya ya Utengano imetafsiriwa kama Separazione katika lugha ya Kiitaliano, hii inaashiria kuwa fasihi ya Kiswahili imeenea hadi mataifa mengine.





Mchango wa Tafsiri katika Fasihi Linganishi ya Kiswahili
Mbali na mchango wa Tafsiri katika Fasihi ya Kiswahili lakini pia Tafsiri imekuwa na mchango mkubwa sana katika Fasihi Linganishi ya Kiswahili, miongoni mwa mchango wa Tafsiri katika Fasihi Linganishi ya Kiswahili ni pamoja na:
Tafsiri hutusaidia kujua na kuliganisha tamaduni za jamii nyingine na ile iliyoandikiwa tafsiri. Kwa mfano katika Tamthilia ya NITAOLEWA NIKIPENDA (I Will Marry When I Want) iliyo andikwa na Ngugi Wa Thiong’o na kutafsiriwa na Crement M. Kabugi (1982). Tamthilia hii imetungwa katika mazingira ya jamii ya Kikuyu, hivyo Tafsiri ya tamthilia hii imesaidia kujua utamaduni wa Wakikuyu. Kwa mfano katika ukurasa wa 65, tunaweza kuona jinsi ndoa ya Kikuyu inavyofungwa, utaratibu wa utoaji mahari pamoja na nyimbo ziimbwazo wakati wa sherehe.
Pia kupitia Tafsiri tunaweza kujua historia ya jamii husika. Katika Tafsiri ya Tamthilia ya NITAOLEWA NIKIPENDA tunaona historia ya Taifa la Kenya tangu wakati wa ukoloni hadi wakati wa Uhuru. Kwa hiyo hapa tunaelewa yale yote wananchi wa Kenya waliyoyapitia wakati wa Ukoloni, kwa mfano katika uk. 32 mwandishi anaonesha adha walizopitia wananchi wa Kenya katika harakati za kupigania uhuru na baadae wakafanikiwa, uk 33. Pia tunaona katika uk. 34 wananchi wanaingia katika kipindi kingine cha uhuru lakini bado wanaendelea kupata adha zilezile kama walizozipata wakati wa Ukoloni.
Tafsiri husaidia kukuza Fasihi ya lugha lengwa. Kupitia Tafsiri, Fasihi ya lugha lengwa inanufaika na kuingizwa vipengele kadhaa vya lugha hususani misemo au methali ambazo hazikuwepo katika lugha lengwa, hivyo kwa kutafsiri misemo hii lugha lengwa nayo pia itakuwa imenufaika na misemo hiyo. Kwa mfano, msemo; “when axes are kept in a one basket they must necessarily knock agaist each other” umefasiriwa kama;“vyuma vikiwa katika gunia moja havikosi kugongana” uk. 24. Kwa hiyo tunaweza kuwa tumeongeza msemo mwingine katika Kiswahili kupitia Tafsiri hii.
Vilevile tafsiri imeongeza idadi ya machapisho ya vitabu vya Fasihi ya Kiswahili na hivyo itakuwa imeimarisha na kukuza fasihi ya Kiswahili nchini Tanzania. Mfano; tamthiliya ya JULIASI KAIZARI (Julius Caesar) (1963) na tamthiliya ya MABEPARI WA VENIS (The Merchant of Venis) (1969) iliyotafsiriwa na Mwalimu Julius K. Nyerere, WIMBO WA LAWINO (Song of Lawino) iliyotafsiriwa na Paul Sozigwa (1975), riwaya ya UHURU WA WATUMWA (The Freeing of the Slaves in East Africa) iliyotafsiriwa na East African Literature Bureau (1967), NITAOLEWA NIKIPENDA (I Will Marry When I Want) iliyotafsiriwa na Crement M. Kabugi (1982), Riwaya ya BARUA NDEFU KAMA HII iliyoandikwa na Mariama Bâ katika lugha ya kifaransa (Une si longue lettre) ikatafsiriwa katika lugha ya Kiingereza na Kiswahili na Professor Maganga.
Pia tafsiri hutusaidia kujua itikadi ya mwandishi na pengine itikadi ya jamii husika. Kwa muktadha wa tamthilia ya Nitaolewa Nikipenda tunaona mwandishi anapinga sana tamaduni na  mtindo wa maisha ya kimagharibi ikiwa ni pamoja na dini za kigeni, lugha zao na mambo yote yaliyoletwa na Wakoloni mfano katika ukurasa wa tano (uk 5).



Kama unahitaji huduma ya kuandikiwa makala katika tovuti yako, au huduma yoyote basi wasiliana nami kupitia:-
SIMU:         +255 755 987 604, +255 789 198 345
E-MAIL:    reubentanzania@gmail.com



Hitimisho
Katika kazi hii tumeangalia vitabu vya Fasihi ya Kiswahili vilivyotafsiriwa, tumeangalia mchango wa Tafsiri katika Fasihi ya Kiswahili na kugusia kwa uchache mchango wa tafsiri katika Fasihi Linganishi. Kwa hiyo kulingana na kazi hii tunaweza kuona mchango na nafasi ya tafsiri katika taaluma ya Fasihi ya Kiswahili, hivyo kuna ulazima mkubwa kwa mtu anayeshughulika na Tafsiri awe ni mjuzi wa Fasihi, hii ni kwa lengo la kuzalisha zao bora la Tafsiri ya Kifasihi. Lakini pia kuna ulazima mkubwa kwa mtaalamu wa Fasihi Linganishi kujua taaluma ya Tafsiri kwa sababu anapofanya ulinganishi kati ya tafsiri na kazi za kifasihi ni lazima uwe na uelewa wa kutosha juu ya taaluma ya Tafsri. Kwa hiyo Fasihi Linganishi na Tafsiri kimsingi ni taaluma zinazoshikamana kuliko kuachana.






MAREJELEO
Mwansoko, H.J.M na wenzake (2006) .Kitangulizi cha Tafsiri, Nadharia na Mbinu. TUKI. Dar-es-salaam
Remak, H.H. (1971). Comperative literature: Its Definition and Function. Carbondale:  Southern Illinois.
Wamitila, K. W. (2003) Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus Publication
Wa Thiong’o, N. & Wa Mirii (1982). I Will Marry When I Want. East African Educatinal Publishers: Nairobi.
Wa Thiong’o, N. & Wa Mirii (1982). Nitaolewa Nikipenda. East African Educatinal Publishers: Nairobi.

MUINGILIANO KATI YA SEMANTIKI NA PRAGMATIKI---ACADEMICIAN BLOG

UTANGULIZI Maana ya Semantiki Richmond (2012   anafafanua maana ya Semantiki kwamba ni tawi la isimu ya lugha linalohusu viyambo ...