Jumanne, 11 Desemba 2018

FASIHI LINGANISHI - MKONDO WA KIMAREKANI


MKONDO WA KIMAREKANI KATIKA FASIHI LINGANISHI
Tangu Marekani ilivyoanza kujiingiza katika fasihi linganishi, huonesha kwa nguvu kuwepo kwa mipaka iliyopo katika mkondo wa kifaransa. Walipenda kuendeleza fasihi linganishi kwa kuikuza kwa maneno mbalimbali katika sanaa na fasihi kwa ujumla, kukua na kujifunza ulinganishi katika nchi ya marekani. Vilevile kulikuwa na mawazo ya waasisi katika chuo kikuu cha Marekani, walifungua dirisha la kuzalisha fasihi iliyoambatana na muunganiko wa mawazo tofautitofauti tangu mwanzo wa historia ya marekani.
Maendeleo ya nadharia ya fasihi linganishi yaliendana sambamba na mawazo ya waasisi kama vile Henry Remark na Rene Wellek. Mwanzilishi wa shule ya kimarekani aliyejitokeza katika nusu ya karne ya 20 alikuwa ni Henry Remark. Mwasisi huyu anasema fasihi linganishi huwa haifungamani na taaluma inayojitegemea bali huwa na mwingiliano kati ya taaluma moja au sehemu husika. Vilevile anaendelea kueleza kuwa ulinganifu huwa unajitokeza kati ya fasihi mbili au zaidi tofauti na kazi ya fasihi na taaluma nyingine kama vile muziki, uchoraji, falsafa, utaalamu wa ujenzi wa nyumba, dini, saikolojia, hesabu, fizikia na kemia.
Mtazamo huu ulikuwa tofauti na mkondo wa kifaransa. Mkondo huu ni wa kimapinduzi kwa vile walilenga kukosoa mitazamo ya kifaransa na kijerumani. Kasoro kubwa waliyoiona ni kuegemea katika misingi ya kinadharia katika kutazama na kuchanganua masuala ya kisanaa.
Waasisi wa mkondo wa kimarekani Henry Remak, Robert Clement na Rene Welleck wamekuwa na mawazo juu ya nadharia hii kama ifuatavyo;
Kwa mujibu wa Henry Remak ambaye anatambulika kama baba wa mkondo wa kimarekani mwaka 1971 yeye alisema, fasihi linganishi kama uwanja wa kifasihi unao husika na uchunguzi na mahusiano ya kifasihi nje ya mipaka ya nchi moja, pia kati ya fasihi na fani nyinginezo.
Remak akaja na mawazo ya kuwepo kwa fasihi linganisi na fasihi ya kitaifa, hakuna utofauti kati ya fasihi linganishi na fasihi ya kitaifa, kutokana na kuwa fasihi linganishi ni fasihi inayo jishugulisha na nje ya mipaka pia fasihi ya kitaifa ni fasihi ambayo huwa na mfanano sana katika tafsiri husika ya fasihi.
Pia anaendelea kusema wazo lingine la uwepo wa fasihi linganishi na fasihi jumla, kuna utofauti kati ya fasihi linganishi na fasihi jumla. Fasihi linganishi hujumuisha elementi ya eneo, muda, aina na watu.  Katika jografia hujumuisha fasihi jumla, ambayo huwa na vipengele vyake kama vile eneo. Pia hujishughulisha na uhusiano kati ya nchi mbili au waandishi wawili katika nchi tofauti au mwandishi mmoja katika kazi zake tofauti.
Hivyo kwa maelezo haya ya Remak tunaweza kusema kwamba fasihi linganishi haiishii kuangalia mahusiano ya kifasihi peke yake bali huangalia mahusiano kati ya fasihi na fani nyingine zisizo za kifasihi. Fasihi linganishi isichukuliwe kama taaluma pekee bali kama kiunganishi baina ya masomo au kama sehemu ya somo.
Rene Wellek, katika kitabu chake cha ``Theory of Literature’’ ambacho pia kiliweza kutafasiliwa kwa lugha ya kiarabu na Sharif Al Sayed (1989) alieleza yafuatayo;
Neno fasihi linganishi kama linavyochukuliwa na shule ya kifaransa ni dhana nzito na yenye kuchanganya katika Nyanja mbalimbali za kuichambua fasihi, hivyo basi jitihada za kupata ujuzi katika shule ya kifaransa juu ya fasihi linganishi ilikuwa duni.
Welleck yeye alipinga uwepo wa mipaka katika kuiangalia fasihi, kwa upande wake anasisitiza kuwa katika kuiangalia fasihi linganishi ni vyema kuihusisha na historia ya fasihi, fasihi ya kitaifa na fasihi jumla. Anaendelea kusema kuwa fasihi linganishi  inakusudia kuondoa fikra au hisia za utaifa na mtazamo finyu lakini haidharau uwepo wa tamaduni tofauti za mataifa na kukua kwake na wala haikusudii kupunguza au kuondoa umuhimu wake lakini tunatakiwa kuwa makini na machaguo yasiyo sahihi ambayo hayaitajiki kwasababu twahitaji vyote yaani fasihi ya kitaifa na fasihi ya kiujumla.

Misingi ya Mkondo wa Kimarekani katika Fasihi Linganishi.
(i). Fasihi linganishi lazima iambae katika nyanja zingine za kitaaluma na maisha kwa ujumla kama vile historia, muziki, saikolojia dini na tamaduni za jamii nyingine.
(ii). Mipaka ya fasihi linganishi lazima iwe huru kutoka taifa moja na taifa lingine kwa sababu fasihi linganishi inahusisha fasihi mbili au zaidi ni lazima ichangie na kuhimiza mahusiano ya kitaaluma kutoka mipaka ya taifa moja hadi taifa lingine. Remak anasema, pamoja na tofauti za kilugha na kiutamaduni mataifa yote hufanana kwa baadhi ya vitu.
(iii). Fasihi Linaganishi yaweza kuwa na fasihi mbili au zaidi. Kwa mujibu wa wataalamu hawa wanaona kuwa fasihi linganishi ni lazima ilinganishe fasihi mbili au zaidi au fasihi mbili za mwandishi mmoja mfano unaweza kufanya ulinganifu wa kazi za Kezilahabi, Penina Mlama na ibrahim Hussein kwa pamoja. Lakini pia unaweza kufanya kazi ya kulinganisha kazi za mwandishi mmoja kwa mfano, E.Kezilahabi “Rosamistika na dunia uwanja wa fujo”.
(iv). Lugha inayotakiwa hutumika katika fasihi Linganishi yaweza kuwa lugha ya kikabila au ya kikanda ilimradi lugha hiyo iwe inatumika katika lugha zote ambazo zaweza kuwa mbili au zaidi.
(v). Fasihi Linganishi hujikita katika kutumia mbinu za kiuhalisia, kiutendaji na kiuhakiki kuhusu kufaa au kutofaa kwa sanaa za ulimwengu. Fasihi ya kitaifa haitengwi na fasihi jumla. Fasihi Linganishi haina maana au haitastawi kama itawekewa mipaka na kuwa taaluma ya fasihi peke yake

Nyanja za Kiuchunguzi.

  • Usambamba 

Hii inakwenda tofauti na taathira ya wafaransa, uwanja huu unaonesha kuwa kuna kufanana au kulingana kati ya fasihi za watu tofauti ambayo mabadiliko yao ya kijamii yanafanana bila kujali kwamba kunakuathiriana kwa karibu au kuna uhusiamo wa moja kwa moja.
Mfano mahusiano ya kisiasa na ya kijamii wakati wa ukabaila yalipelekea kufanana kwa mkondo wa mawazo, sanaa na fasihi katika sehemu mbalimbali za dunia.
Uwanja huu unaiangalia misingi inayoonyesha sifa za usanii wa mwandishi na mwandishi, hauzingatii umuhimu wa kuhusianisha.
Haizipi umuhimu taathira, kuna uwezekano wa kuzishughulikia matini za kifasihi bila kuonana/ kuwasiliana kwa aina yoyote bali kwa mazingira au uhalisia unaofanana.
Kama taathira zipo katika matini za kifasihi umuhimu wake haupo katika taathira yenyewe isipokuwa kwa mazingira. Kama mazingira hayataruhusu tathira kuwa yenye tija bali taathira haitatokea

  • Mwingiliano Matini

Maana ya mwingiliano matinni kwa mujibu wa Enani, ni uhusiano kati ya matini mbili au zaidi katika kiwango ambacho kinaathiri usomaji wa matini mpya. Matini inayoathiri inachanganywa na maudhui ya matini inayo athiriwa, yaani kuathiriana kwa waandishi wawili.
Kwa mjibu wa Leon, S, Roudiz anasema ni mbadilishano wa karibu wa mfumo wa ishara baina ya matini. Yaani ni kutumia mfumo mmoja wa uandishi badala ya mwingine.
Hivyo basi wanasisitiza mwingiliano wa matini kwa kuwa kila msomaji atachukua sehemu Fulani ambayo inaendana na utamaduni wake, lugha na ujuzi kutoka katika matini. Yani:
-Matini mpya au ngeni inaingizwa kwenye matini ya zamani,
-Matini mpya inasomwa kwa kuzingatia matini ya zamani,
-Ni mchakato endelevu wa kuboresha matini ya zamani.
-Matini ya zamani inakuwa ni malighafi ya kutengeneza matini mpya.

Ubora wa Mkondo wa Kimarekani
(i). Walihusisha fasihi simulizi na fasihi andishi, mtazamo huu ulijikita kuangalia fasihi kwa ujumla tofauti na mitazamo mingine kama vile mtazamo wa kifaransa ambao ulijikita kuangalia fasihi andishi tu, mfano katika fasihi simulizi walijikita kuangalia vipengele vya fasihi simulizi kama vile muziki.
(ii). Mtazamo huu unaweza kufanya ulinganifu katika kazi mbili ambazo zilitumia lugha moja kutoka mataifa mawili tofauti mfano kazi iliyoandikwa kwa kiswahili nchini kenya ukilinganisha na kazi za kiswahili nchini Tanzania mfano kazi ya Wamitila “bina-adam” na Kezilahabi “Nagona”. Hivyo wamefanikiwa kutenganisha fasihi linganishi na suala zima la utaifa. Ambapo mtazamo huu ulijikita katika mtazamo wa kimataifa.
(iv). Walitenganisha taaluma ya fasihi kutoka katika vizingiti au vikwazo vya kisiasa, kitabaka na lugha.
(v). Wanasisitiza kuwa katika kufanya ulinganifu, mlinganishaji asifungwe na njia moja ambapo wanadai kuwa njia ya kihistoria sio njia pekee inayotumika katika kulinganisha kazi za kifasihi kutoka jamii au mataifa tofauti.

Udhaifu wa Mkondo wa Kimarekani
(i). Mkondo huu unachanganya fasihi na fani au taaluma nyingine kama vile muziki, falsafa, saikolojia, uchoraji, hisabati na sayansi ya jamii. Kama lilivyo jina la taaluma yenyewe yaani fasihi linganishi, inaonyesha kuwa inahusika na ulinganishi wa kazi za kifasihi. Kuingiza taaluma za falsafa, saikolojia hisabati au sayansi ya jamii katika fasihi linganishi ni kuchanganya taaluma.
(ii). Mkondo huu unachanganya fasihi linganishi na fasihi jumla kwa madai kwamba zote zinahusika na ujifunzaji wa somo moja yaani fasihi. Lakini kiuhalisia, taaluma ya fasihi linganishi na fasihi jumla hazifanani ingawa zote ni taaluma za fasihi. Fasihi linganishi inahusika na ulinganishi wa kazi mbalimbali za fasihi lakini fasihi jumla haihusiki na ulinganishaji wa kazi za kifasihi. Inaangalia kazi za fasihi kwa ujumla wake na umaarufu wa kazi hizo duniani.
(iii). Usanii unatofautiana kutegemeana na taifa na historia. Inategemea mambo ya kifasihi yanayozungumziwa na historia ya kila jambo kama inafanana au siyo. Hii inatokana na mawazo yao katika uwanja wa usambamba ambapo wanasema kuwa “kuna kufanana au kulingana kati ya fasihi za watu tofauti ambao mabadiliko yao ya kijamii yanafanana bila kujali kwamba kuna kuathiriana kwa karibu au kuna uhusiano wa moja kwa moja baina ya watu hao.” Ukweli ni kwamba, jamii zinaweza kuwa zimepitia katika mfumo wa kijamii unaofanana na jambo linalozungumziwa linaweza kuwa moja. Lakini, kama historia ya jambo hilo inatofautiana kati ya taifa moja na taifa jingine, sanaa yake pia itatofautiana.
(iv). Mkondo huu haukuzingatia suala la fasihi kuathiri au kuathiriwa na kitu kingine wakati kiuhalisia fasihi inaweza kuathiri au kuathiriwa na vitu kama vile utamaduni na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
(v). Kutumia fasihi ya Ulaya kama kielelezo cha fasihi jumla ni udhaifu. Hii inatokana na jinsi Remak alivyoifasili fasihi jumla kuwa ni “dhana inayotumika kuelezea machapisho ya fasihi ngeni kwa kutumia tafsiri ya Kiingereza”. Hii inaonyesha kuwa alikiangalia zaidi Kiingereza ambayo ni lugha ya Kiulaya na kutotilia maanani lugha zingine.
(vi). Udhaifu mwingine upo katika fasili yao ya fasihi linganishi kuwa ni taaluma inayohusika na kulinganisha kazi mbili au zaidi. Ni ngumu kulinganisha kazi zaidi ya mbili kwa sababu katika ulinganishaji wa kazi kwa mfano kazi tatu, kutakuwa na sifa ambazo zinafanana kwa kazi mbili na katika kazi ya tatu sifa hizo hazipo. Kwa hiyo inakuwa ngumu kutoa hitimisho juu ya kazi hizo kwani zinafanana kwa sifa zipi na zinatofautina katika sifa zipi.
MAREJELEO
Remak. H.H. (1971) “Comparative Literature :Its definition and function’’ (Method and Parspective), Edited by Newton.B.Stalknecht and Horst Frenz, USA October 1973. http://www.ocia.org
Rene H.H. Wellek, First  Edition (1949) Theory of Literature. Published by Suprome Council for Literatures, Arts and Social Science .Domascus 1972.
Wamitila K.W (2003), Kamusi ya Fasihi,Istirahi na Nadharia, Nairobi: Kenya.  



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

MUINGILIANO KATI YA SEMANTIKI NA PRAGMATIKI---ACADEMICIAN BLOG

UTANGULIZI Maana ya Semantiki Richmond (2012   anafafanua maana ya Semantiki kwamba ni tawi la isimu ya lugha linalohusu viyambo ...